![]() |
| Image by: Harbin Clinic |
Utakubaliana na mimi kwamba, kitendo cha mtu kubanwa na haja ndogo siyo kitu cha hiyari kwamba sasa mtu anaamua ngoja nibanwe na mkojo, hili ni jambo la asili na ni matokeo ya vyakula, matunda au vinywaji tunavyotumia. Kwa lugha nyingine tumekuwa tukiita kuwa ni wito wa asili au nature’s call.
Yawezekana mtu akawa katika mkutano, safarini, akawa katika
mitandao ya kijamii anachati au popote pale akiwa anafanya jambo fulani na
kutokana na jambo hilo, mtu akaendelea kujibana na kutokwenda kuyapunguza maji-taka mwili, haya kutoka katika kibofu cha mkojo kwa kutoa kipaumbele kwa shughuli
anayoifanya kuliko kusikiliza kwanza wito huu wa asili 'kuwa kibofu chake kimejaa.
Mambo haya tunayafanya sana, utasikia, mkojo umenibana kweli,
ila ngoja nimalizie hii kazi halafu niende kujisaidia, hivi ndivyo watu wengi
wafanyavyo kimazoea kitu ambacho hakishauriwi kitabibu na kwa afya ya mwili wako.
Kutokana na vyakula na vinywaji tunavyotumia katika milo yetu kila wakati, kibofu cha mkojo
huanza kujaa mkojo, unaojitengeneza wakati vyakula vinachaguliwa (Kuchakatwa) na mwili, hivyo mkojo unapofikia karibu mililita 50 mpaka 500 mtu huyo husika huanza
kuhisi hitaji la kwenda haja ndogo (kukojoa).
Kibofu cha mkojo kimezungukwa na vigunduzi asili (Receptors)
vinavyopeleka taarifa katika Ubongo kuonyesha kuwa kibofu cha mkojo kimekaribia
au kimejaa, baada ya taarifa hizi kufika katika ubongo, ubongo unatoa taarifa
katika kibofu cha mkojo ili kiweze kushikilia mkojo huo kwa kuikaza misuli
maalumu (Sphincters) mpaka hapo muda wa wewe kwenda kukojoa utakapofika.
Kibofu cha mkojo hufanya kazi kwa mfumo wa kujiendesha wenyewe
yaani, automatic, kitendo cha mtu kupuuzia kwenda kukojoa husababisha Ubongo
upate usumbufu wa taarifa za kujaa kwa kibofu cha mkojo na kwa kuwa Ubongo nao
hutuma taarifa katika kibofu cha mkojo kusema kuwa mkojo uendelee kushikiliwa
mpaka muda muafaka utakapofika, itafika kipindi uwezo wa ubongo kutoa taarifa
hizi na pia uwezo wa vigunduzi asili (Receptors) vilivyoko katika kibofu cha
mkojo kupoteza uwezo wake tena wa kufanya kazi hizo au uwezo kuwa mdogo.
Matokeo yake ni mtu siku kweli anahitajika kuvumilia kidogo ili
afike sehemu inayostahihi kujisaidia, lakini hawezi tena na kujikuta muda mdogo
tu….mtu tayari kaloanisha nguo yake.
Mpenzi msomaji, mtu kujibana na kupuuzia kwenda haja ndogo mara
kwa mara husababisha uwezo wa kibofu chake cha mkojo kushindwa kujitawala upotee.
Pia kama uwezo wa neva zinazopeleka taarifa kwenye ubongo kuhusu
mabadiliko/ujazo wa kibofu cha mkojo zitaharibika, basi misuli maalumu ya
kubana mkojo (sphincter) itashindwa kuachia na matokeo yake mtu ataendelea
kukaa na mkojo katika kibofu chake kwa muda mwingi zaidi kitu ambacho ni hatari
kwa afya yake.
Endapo mkojo huu utashindwa kutoka, utatengeneza mazalia ya
bakteria na kukusababishia magonjwa ya kibofu (bladder infection), kama vile U.T.I
(Urinary Tract Infections), na pia huweza kusababisha magonjwa ya figo na
mchafuko wa damu, (bacteremia).
Kuna hali huwa inajitokeza kwa baadhi ya watu, yawezekana
alikuwa kabanwa na mkojo au alikuwa hajahisi kwenda kukojoa, ila akinywa maji
au akisikia sauti ya maji yanachuluzika mfano maji yakitoka bombani, basi
atahisi kwenda kukojoa.
Mpenzi msomaji, ni vyema tukawa wasikivu pale mtu unapobanwa na haja (mkojo), hii ni kwa ajili ya afya ya kibofu chako cha mkojo lakini pia ni kwa
ajili ya afya yako kwa ujumla. Kama unalo tatizo, usisite kuonana na wataalamu
wa afya..

No comments:
Post a Comment